28 Septemba 2013 - 20:30
Mazungumzo baina Obama na rais wa Iran

Rais Barack Obama wa Marekani amefanya mazungumzo ya simu na mwenzake wa Iran Bw Hssan Rouhani kuhusu juhudi zinazoendelea za kutatua suala la nyuklia la Iran. Kupitia hotuba yake kwenye televisheni, Obama amethibitisha kufanya mazungumzo na Rouhani, yakiwa ni mazungumzo ya kwanza kati ya marais wa nchi hizo mbili kwa zaidi ya miaka 30 iliyopita.

Ripoti ya ABNA- Baada ya mazungumzo hayo, Obama amesema ana imani watafikia suluhisho la mpango wa nyuklia wa Iran. Marais hao wawili wamewataka wawakilishi wao kufanya kazi kwa ufanisi na kuendelea kushirikiana na nchi nyingine kwa lengo la kufikia makubaliano kuhusu suala la nyuklia.

Ofisi ya rais wa Iran pia imethibitisha kufanyika kwa mazungumzo hayo kupitia ukurasa wake wa Twitter. Alhamisi, waziri wa mambo ya nje wa Iran Javad Zarif alikutana na wenzake kutoka nchi za Uingereza, China, Ufaransa, Russia na Marekani kuzungumzia mpango wa nyuklia wa nchi hiyo.