Raia wasiopungua thelathini na wanne wameuliwa kwa kukatwakatwa kwa mapanga na mashoka na watu wanaosadikiwa kuwa ni waasi kwenye kijiji cha Ahili kilichopo kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo.
Afisa mmoja wa kijiji hicho amesema kuwa mauaji hayo yalifanyika hapo jana katika mfululizo wa mashambulio yanayoelekezwa kwa raia. Mkuu wa usimamizi wa utawala katika kijiji cha jirani amesema waasi walikilenga kijiji cha Ahili kilichopo umbali wa kilometa 10 kutoka mji wa Oicha katika jimbo la Beni. Watu wanaotuhumiwa kuwa waasi walianza kuwashambulia wanakijiji saa moja jioni wakati wanakijiji walipokuwa kwenye mashamba yao na hivyo ilikuwa vigumu kwao kupiga mbiu ya mgambo. Viongozi wa serikali pamoja na asasi za kiraia zimelilaumu kundi la ADF kwa mauaji hayo. Kundi hilo la siri liliundwa mnamo miaka ya 90 kupambana na serikali ya Uganda. Mpaka sasa raia zaidi 250 wameshauawa tokea mwezi wa Oktoba katika jimbo la Beni na maeneo jirani.
Yafaa kuashiria kuwa kutokana na utajiri na rasilimali za nchi ya Congo waatu wengi wamekuwa wakitamani mali za nchi hiyo na hivyo kusababisha uasi na uporaji wa mali na maeneo muhimu.