5 Juni 2025 - 16:22
Radiamali ya Wapalestina kuhusu Kura ya Veto juu ya Azimio la Baraza la Usalama: Hatua ya Marekani ni Kutoa Uhalali wa Mauaji ya Kimbari huko Gaza

Ofisi ya Habari ya Serikali ya Palestina katika Ukanda wa Gaza imelaani vikali kura ya veto iliyowekwa na Marekani dhidi ya azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, na kuitaja kama ishara ya wazi ya uungaji mkono wa Washington kwa uhalifu unaotekelezwa na utawala wa Kizayuni. Taasisi hiyo imesisitiza kuwa hatua hiyo itaongeza mgogoro wa kibinadamu huko Gaza na kusababisha kuongezeka kwa mauaji ya raia wasio na hatia. Imeyataka jumuiya ya kimataifa kuchukua hatua za haraka na madhubuti ili kuokoa maisha ya watu wasiokuwa na hatia katika eneo hilo.

Kwa Mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (a.s) -ABNA- Ofisi ya Habari ya Serikali ya Palestina katika Ukanda wa Gaza imelitaja kura ya veto ya Marekani dhidi ya azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuwa ni doa jipya la fedheha katika rekodi ya maadili ya Marekani, na imelilaani vikali tukio hilo kwa maneno makali zaidi.

Ofisi ya Habari ya Serikali ya Palestina katika Ukanda wa Gaza imetoa taarifa kali ya kulaani hatua ya Marekani ya kutumia kura ya veto dhidi ya azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Taarifa hiyo imesema:

“Tunalaani vikali matumizi ya kura ya veto na Marekani dhidi ya azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lililokuwa linataka kusitishwa kwa mapigano mara moja na milele katika Ukanda wa Gaza na kuhakikisha kuingia kwa misaada ya kibinadamu bila vikwazo vyovyote, wakati ambapo eneo hili linakabiliwa na janga kubwa la kibinadamu na jinai ya mauaji ya kimbari inayoendelea kufanywa na wavamizi.”

Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Habari la Palestina, Shahab, taarifa hiyo imeongeza kuwa:

“Veto hii ya aibu na ya kuaibisha ni ushahidi wa wazi wa uungaji mkono wa Marekani kwa mashine ya kivita ya utawala wa Kizayuni na msaada wa kisiasa kwa jinai zinazotekelezwa dhidi ya watu wa Palestina, hususan watoto, wanawake, wagonjwa na wazee.”

Taarifa hiyo imebainisha kuwa hatua ya Marekani ya kutumia kura ya veto siyo tu doa la maadili katika historia ya Marekani, bali pia ni ushiriki wa moja kwa moja katika jinai ya mauaji ya kimbari. Pia imeeleza kuwa:

“Kisingizio na maelezo yaliyotolewa na wawakilishi wa Marekani hayapaswi kuchukuliwa kwa njia yoyote ile isipokuwa kama juhudi za kuhalalisha mauaji ya kimbari, uvamizi, njaa na maangamizi ya watu wa Palestina, jambo ambalo linakinzana wazi na sheria za kimataifa, mkataba ya kibinadamu, na misingi ya haki na usawa.”

Taarifa hiyo imeendelea kwa kusisitiza kuwa Marekani inahujumu jitihada zote za kimataifa za kusimamisha mashambulizi dhidi ya raia wa Ukanda wa Gaza na kuokoa maisha ya zaidi ya Wapalestina milioni 2.4 walioko chini ya mzingiro, wasiokuwa na upatikanaji wa maji, chakula na dawa kutokana na mabomu na njaa.

Katika hitimisho, taarifa hiyo imepongeza misimamo ya nchi zilizopiga kura kuunga mkono azimio hilo na kutaka hatua za haraka na thabiti zichukuliwe na Jumuiya ya Kimataifa, Umoja wa Mataifa na taasisi zote za haki za binadamu na misaada ya kibinadamu kwa ajili ya kuokoa maisha ya watu wasio na hatia katika Ukanda wa Gaza.

Taarifa hiyo imetolewa kufuatia kura ya veto ya Marekani dhidi ya rasimu ya azimio la Umoja wa Mataifa kuhusu sitisho la mapigano huko Gaza.

Taarifa za awali kutoka tovuti ya habari ya Marekani, Axios, zilisema kuwa Washington ilikuwa imeshaarifu utawala wa Kizayuni kwamba itatumia kura ya veto kuzuia azimio hilo. Nchi 10 wanachama wa Baraza la Usalama walikuwa wametayarisha rasimu hiyo kwa ajili ya kupigiwa kura.

Kwa mujibu wa Al Jazeera, azimio hilo lilitaka kuondolewa kwa vikwazo vyote vinavyokwamisha misaada kuingia Gaza na kutoa ruhusa kwa Umoja wa Mataifa na washirika wake kusambaza misaada na kurejesha huduma za msingi katika eneo hilo kwa mujibu wa sheria za kimataifa.

Tangu Oktoba 7, 2023, mashambulizi ya utawala wa Kizayuni yamesababisha vifo vya zaidi ya watu 54,000 na kujeruhi wengine wapatao 125,000, huku wengi wakilazimika kuhama makazi yao. Watu wa Gaza wanakumbwa na njaa kali, ukosefu wa maji, chakula, dawa na mahitaji ya msingi ya maisha.

Tags

Your Comment

You are replying to: .
captcha