Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (a.s) –ABNA– hivi karibuni Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni, alielekea Washington na kutangaza kuwa lengo la safari yake ni kufanya mazungumzo na Donald Trump, Rais wa Marekani, kuhusu mafaili muhimu ikiwemo suala la Iran.
Wachambuzi wa kisiasa walieleza kuwa safari hiyo kwa hakika ilikuwa ni juhudi ya Netanyahu kumshawishi Trump kuanzisha vita dhidi ya Iran na kuratibu kikamilifu na Ikulu ya Marekani kuhusu mpango wowote katika muktadha huo.
Hata hivyo, mwishoni mwa mkutano huo, Trump alitangaza kutofikiwa kwa makubaliano na Netanyahu kuhusu faili la Iran, akidai kuwa msimamo wake ulikuwa kusisitiza matumizi ya diplomasia na kuendeleza mazungumzo na Iran.
Kipaumbele ni maslahi ya Trump!
Wissam Nasif Yassin, mwandishi na mchambuzi wa uhusiano wa kimataifa kutoka Lebanon, katika mahojiano na ABNA kuhusu matokeo yanayoweza kutokea ya safari ya Netanyahu kwenda Washington na mkutano wake na Rais wa Marekani, alisema: “Angalau kwa sasa haionekani kuwa kuna makubaliano yoyote kati yao, hasa ikizingatiwa kuwa hawakufanya mkutano wa waandishi wa habari wala kutoa taarifa rasmi.”
Mtaalamu huyo wa Lebanon alisisitiza kuwa ni wazi maslahi ya Trump katika mazingira ya sasa ndiyo yaliyopewa kipaumbele, kwani bado ana mashaka kuhusu kuingia vitani na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Kwa sasa, mazungumzo ni jambo la lazima kwa Trump. Ikiwa atapata mafanikio, ataepuka vita; lakini ikiwa mazungumzo hayataleta maendeleo, anaweza kujaribu kuandaa hoja dhidi ya Iran ili, kwa madai fulani, kuhalalisha kuingia vitani.
Kipaumbele ni mazungumzo
Kuhusu uwezekano wa vita kati ya Iran na Marekani, alisema kuwa hali bado inaelekea zaidi kwenye suluhisho la mazungumzo lililo imara, ingawa chaguo la vita haliwezi kuondolewa kabisa. Hata hivyo, kwa kuzingatia uwezo wa Iran, utayari wake na uungwaji mkono wa wananchi kwa uongozi wake, inaonekana kuwa ni vigumu kuthubutu kutumia chaguo la kijeshi.
Uwepo wa manowari za kubeba ndege ni fursa kwa Iran
Akichambua hatua ya Marekani ya kutuma manowari mpya ya kubeba ndege, USS Gerald R. Ford, baada ya mkutano na Netanyahu, Dkt. Yassin alisema: “Jamhuri ya Kiislamu iko tayari kwa vita, na jambo hili lenyewe linapunguza uwezekano wa kutokea kwa vita.”
Aliongeza kuwa, ingawa manowari hizo ni tishio kwa Iran, lakini kwa kuzingatia kuwa karibu wanajeshi 5000 waliopo humo wako katika masafa ya kufikiwa na mashambulizi ya Iran, hali hiyo pia inaweza kuhesabika kama fursa kwa Iran.
Kuhusu athari za mvutano wa kijeshi katika eneo la Mashariki ya Kati, alieleza kuwa nchi nyingi za eneo hilo hazitaki vita, kwa sababu wakati wa vita zitakuwa katika masafa ya mashambulizi ya Iran. Aidha, akasema kuwa ikiwa – Mungu apishe mbali – Iran itashindwa, eneo lote linaweza kujikuta katika makucha ya Israel, jambo ambalo nchi kama Saudi Arabia, Turkey, Qatar na Egypt hakika hazilitaki.
Your Comment