Kwa Mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) –ABNA– Shirika la Ujasusi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu wa Iran (IRGC) limetangaza kuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inaona uvukaji wa mipaka myekundu katika maeneo ya Lebanon na Gaza kuwa ni sawa na kuanzishiwa vita vya moja kwa moja pamoja na kuhatarishwa kwa usalama wake wa taifa na wa Muqawama wa Kiislamu.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa Iran ina azma thabiti ya kutekeleza operesheni za kujihami, ikiwemo kuchukua hatua kali na za maamuzi, kufungua medani mpya za mapambano, na kudumisha mkakati wake kuhusu Mlango wa Bahari wa Hormuz endapo maslahi yake au ya mhimili wa Muqawama yatatishiwa.
Shirika hilo limesisitiza kuwa litajibu kwa nguvu hatua yoyote itakayoonekana kuvuka mipaka hiyo, likionya kwamba matokeo ya vitendo hivyo yatakuwa makubwa kwa wahusika wake.
Taarifa hiyo imehitimishwa kwa kauli inayosema: "Yeyote anayepanda upepo, atavuna tufani." Kauli ambayo imefasiriwa na wachambuzi kuwa ni onyo kali kwa wale wanaoweza kuchukua hatua zitakazoongeza mvutano katika eneo la Mashariki ya Kati.
Your Comment