Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (a.s) -ABNA-, leo tarehe 22 Bahman 1404 / 11 February 2026, mamia ya miji na vijiji katika majimbo mbalimbali ya Iran yalishuhudia sherehe za kuadhimisha miaka 47 ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu.
Mamilioni ya wananchi walijitokeza barabarani katika zaidi ya maeneo 1400 nchini kote, wakiitikia wito wa Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu wa Iran na kuadhimisha siku hii tukufu ya kitaifa.
Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa, zaidi ya waandishi wa habari 7,000 wa ndani na wa kimataifa waliripoti tukio hilo kubwa. Wakati huohuo, vyombo vya habari vya nje vilirusha matangazo ya moja kwa moja ya maandamano hayo ya mamilioni.
Mashirika ya habari kama Reuters, Agence France-Presse (AFP) pamoja na runinga za kimataifa kama Al Jazeera, Al Mayadeen na vyombo vingine, vilianza kurusha matangazo ya moja kwa moja tangu mwanzo wa maandamano hayo.
Shirika la habari la Associated Press katika ripoti yake lilieleza kuwa ushiriki mkubwa wa wananchi katika Tehran na miji mingine ya Iran ni ishara ya mshikamano wa kitaifa na uungaji mkono wa wananchi kwa mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu, na likasisitiza ushiriki wa watu kutoka tabaka zote za jamii.
Gazeti la Marekani The New York Times pia lilielezea maandamano ya 22 Bahman kama “onesho la kusimama kidete”, likiandika kuwa licha ya uwepo wa manowari na vikosi vya Marekani katika eneo hilo, Iran iliadhimisha kwa nguvu kumbukumbu ya Mapinduzi ya Kiislamu ya mwaka 1979, huku wananchi wakifanya maandamano makubwa kote nchini.
Kwa ujumla, vyombo vya habari vya kimataifa vimetafsiri tukio la 22 Bahman kama ujumbe wa wazi wa mshikamano wa wananchi wa Iran, uimara wa taifa hilo, na uungaji mkono wao kwa misingi ya Mapinduzi ya Kiislamu licha ya shinikizo na vitisho vya nje.
Your Comment