Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (as) -ABNA- Kongamano la kimataifa lenye kaulimbiu "Imam Hussein (as) kwa Mtazamo wa Dini na Madhehebu" limefanyika katika mji Mtukufu wa Karbala, Iraq, likiwakutanisha wanazuoni na watafiti kutoka mataifa mbalimbali kujadili nafasi ya Imam Hussein (as) katika kuimarisha maadili ya haki, amani na mshikamano wa kibinadamu.
Katika kongamano hilo, kitabu kipya cha Profesa Chris Hewer, mtafiti wa masuala ya Ashura na mwanazuoni Mkristo kutoka Uingereza, kilizinduliwa rasmi. Kitabu hicho kinamwelezea Imam Hussein (as) kama mpiganiaji wa haki na mfano wa kudumu wa kusimama dhidi ya dhulma.
Akizungumza katika hafla hiyo, Profesa Hewer alisema kuwa Imam Hussein (as) si kiongozi anayehusiana na Waislamu pekee, bali ni urithi wa wanadamu wote. Alibainisha kuwa Mapinduzi ya Karbala yanatoa somo lisilo na kifani la kupambana na dhulma, kulinda utu wa mwanadamu na kuendeleza amani na uadilifu katika jamii.
Washiriki wa kongamano hilo, wakiwemo wanazuoni kutoka Misri na Uturuki, walieleza kuwa tukio la Karbala linaendelea kuwa daraja la kuimarisha maelewano kati ya dini na madhehebu mbalimbali. Walisisitiza umuhimu wa kujenga mazungumzo na mshikamano unaozingatia mapenzi kwa Ahlul-Bayt (as) na maadili ya haki na huruma.
Aidha, waliohudhuria walieleza kuwa utamaduni wa kujitolea, mshikamano na huduma unaodhihirishwa katika Arubaini ya Imam Hussein (as) ni ujumbe wenye umuhimu wa kimataifa unaoweza kuchangia katika kujenga jamii yenye haki, amani na mshikamano miongoni mwa watu wa dini na tamaduni tofauti.
Maoni yako